0
Asilimia 96 ya watanania wanamkubali Rais Magufuli, na asilimia 88 ya wananchi Tanzania wameonesha imani ya kuwa Rais Magufuli ataendelea na kasi aliyoanza nayo katika uwajibikaji.


Wananchi hao pia wamevutiwa na uondoaji wa wafanyakazi hewa, utoaji wa elimu bure pamoja na usimamishaji watumishi wa serikali kwa makosa mbalimbali.

Takwimu zilizotolewa kwa vyombo vya habari na shirika la TWAWEZA jana  jijini Dar es salaam kupitia kwa mkurugenzi mtendaji wa wa shirika hilo Aidan Eyakuze, zimebainisha kuwa asilimia 69 ya watanzania wamefurahishwa na uondoaji wa wafanyakazi hewa uliotajwa, asilimia 67 wamefurahishwa na elimu bure huku asilimia 61 wakipendezwa na utumbuaji majipu.

“Kwa ujumla kiwango cha kukubalika kwa Rais Magufuli anakubalika na asilimia 96 ya wananchi. Kiwango hiki kinaendana na viwango vya kukubalika kwa marais wa Tanzania waliopita. Pamoja na hayo, asilimia 88 ya wananchi wana imani kuwa Rais Magufuli ataendelea na kasi aliyoanza nayo, mpaka mwisho wa awamu yake ya uongozi”

Aidha wananchi pia wameonesha viwango vya kukubalika kwa viongozi wao wa kijiji na serikali za mitaa ambapo wenyeviti na watendaji wa vijini wanakubalika kwa asilimia 78, diwani kwa asilimia 74 na mbunge kwa asilimia 68.

Matokeo haya yametolewa na Twaweza kwenye utafiti uitwao "Rais wa Watu. Tathmini na matarajio ya wananchi kwa serikali ya awamu ya tano". 

Muhtasari huo umetokana na takwimu kutoka Sauti za Wananchi, ambapo wahojiwa 1,813 kutoka maeneo yote Tanzania Bara kati ya tarehe 4 Juni na tarehe 20 Juni 2016 walihojiwa.

Aidha Wananchi wengi wanasema serikali ya awamu ya tano imeleta maboresho kwenye huduma nyingi za umma, huku Mamlaka ya Mapato Tanzania ikiongoza kwa asilimia 85 .

Wananchi pia wamesema huduma ni nzuri mashuleni kwa asilimia 75, vituo vya polisi kwa asilimia 74, mahakamani kwa asilimia 73, vituo vya afya asilimia 72 na mamlaka za maji asilimia 67.

Pamoja na kiwango kikubwa cha kukubalika kwa serikali ya awamu ya tano na Rais John Pombe Magufuli, wananchi wapo makini na kanuni za demokrasia na haki na wanataka zifuatwe.

Wananchi nane kati ya kumi (au 80%) wanasema watendaji wa umma waondolewe pale tu panapokuwepo udhibitisho wa vitendo viovu.

Asilimia 75 wanasema kuwa watendaji waondolewe pale wanaposhindwa kufanya kazi zao na siyo wanaposhindwa kufuata maagizo ya Rais.

Post a Comment

 
Top